News

Find what's going on with us

STEPS Tanzania Yafikia Jamii Tanga Kupitia Mradi wa Momentum

STEPS Tanzania kupitia mradi wa Momentum, unaotekelezwa katika Mkoa wa Tanga, imefanikiwa kuendesha vikao vya kufikia jamii na kutoa elimu kuhusu athari za matumizi ya madawa ya kulevya pamoja na mikakati ya kupunguza madhara yatokanayo na matumizi ya madawa ya kulevya (Harm Reduction), hususan kwa wanawake wanaoishi na/au wanaoathirika na matumizi ya madawa ya kulevya katika kata za Mwanzange na Chumbageni.

Vikao hivyo viliongozwa na timu ya Waelimishaji Rika, kwa kushirikiana na Mental Health Coordinator, pamoja na uongozi wa Kata (LGA). Ushirikiano huu uliwezesha kutoa hamasa na elimu kwa wanajamii, kwa lengo la kujenga jamii iliyo salama, yenye uelewa wa kutosha juu ya namna ya kuwahudumia na kuwaunga mkono watu wanaoathirika na matumizi ya madawa ya kulevya bila unyanyapaa.

Akizungumza katika vikao hivyo, Mental Health Coordinator alielezea kwa kina huduma mbalimbali zinazotolewa katika Kliniki ya MAT (Medication Assisted Treatment), na kusisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kuendelea kuwapa ushirikiano watoto wao walioanza matibabu ya MAT. Alisisitiza kuwa kuepuka unyanyapaa ni hatua muhimu inayowasaidia wagonjwa kurejea katika hali bora ya afya ya akili na ustawi wa maisha yao kwa ujumla.

Mbali na hilo, wanajamii walipatiwa elimu juu ya:

Magonjwa ya kuambukizwa kwa kuchangia sindano, yakiwemo VVU

Kifua Kikuu (TB) miongoni mwa watu wanaotumia madawa ya kulevya

Afya ya uzazi na uzazi wa mpango kwa wanawake wanaotumia madawa ya kulevya

 

Aidha, timu ilitekeleza zoezi la kutembelea maeneo hatarishi (Hotspots) kupitia programu ya Moonlight Outreach katika eneo la Sabasaba. Katika matembezi hayo ya usiku, Waelimishaji Rika waliweza:

Kutoa elimu ya VVU na UKIMWI, TB, na Harm Reduction

Kugawa kondomu

Kutoa hamasa kwa waraibu waliokutwa maeneo hayo kufanya uchunguzi wa afya zao na kujiunga na huduma stahiki

Jumla ya wanajamii 105 walihudhuria vikao vya elimu katika Kata ya Chumbageni na Mwenzange. Vilevile, waraibu waliokutwa wakati wa Moonlight Outreach walipewa fursa ya kujiunga na programu za uwezeshaji kiuchumi zinazotolewa na asasi washirika, zikiwemo MUKIKUTE, OYARB, na Gift of Hope. Kupitia Mfuko wa CHAC, huduma pia zinaendelea kuwafikia WAVIU ambao pia ni waraibu wa madawa ya kulevya.



STEPS Tanzania inatoa shukrani na pongezi za dhati kwa ViiV Healthcare pamoja na MUKIKUTE kwa kuendelea kuunga mkono utekelezaji wa programu za kupunguza madhara kwa wanawake wanaotumia madawa ya kulevya na wenza wao katika Mkoa wa Tanga.

Picha mbalimbali za Matukio katika afua hiyo